Na VENANCE JOHN
Watu 18 ambao ni abiria 16, dereva na kondakta wanashikiliwa na Jeshi la Polisi mkoani Mara kwa tuhuma za kumpiga askari wa usalama barabarani aliyekuwa akikagua gari walilokuwa wamepanda.

Tukio hilo lilitokea siku ya Jumatano Septemba 18, 2024, saa 12 jioni. Ofisa Mnadhimu wa Jeshi la Polisi Trafiki Kuu, Butusyo Mwambelo amesema askari huyo alikumbwa na kipigo baada ya kuamuru abiria waliosimama kushuka kwenye gari.
Butusyo Mwambelo amesemea, kondakta wa gari hilo alifunga mlango baada ya askari huyo kuingia ndani ya gari na wote waliokuwa ndani ya gari, akiwamo dereva, kondakta na abiria, walianza kumshambulia askari huyo.
“Askari wetu alikuwa akitekeleza wajibu wake wa kuwataka abiria waliokuwa wamesimama kwenye gari washuke, lakini ghafla walimzonga kwa maneno ya kebehi, na kondakta akafunga mlango wa gari. Ndipo dereva, kondakta na abiria wao wakaanza kumpiga askari akiwa ndani ya gari. Je, kweli tumefika hatua hiyo kama Watanzania?” amesema Mwambelo.
Mwambelo amesema hayo wakati wa operesheni ya ukaguzi wa magari iliyofanyika Septemba 19, 2024, katika Kituo Kikuu cha Mabasi cha Geita na kusisitiza kuwa tukio hilo ni la kusikitisha na halitavumiliwa na kwamba jeshi la polisi limechukua hatua za haraka kuhakikisha wote waliohusika katika tukio hilo watawajibishwa kisheria.
Comentarios